Ticker

7/recent/ticker-posts

MIPANGO YA KUTOKOMEZA UJANGILI KUBORESHWA NCHINI

Kaimu Mkurugenzi Msaidizi Sehemu ya Makosa ya Mazingira na Maliasili Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, Salimu Msemo



NA SIDI MGUMIA, DODOMA

 

Ujangili nchini umeendela kushughulikiwa kwa mbinu mbalimbali kwa ushirikiano wa vyombo vya dola,wanasheria na wadau wengine wa uhifadhi.

Matukio ya ujangili wa tembo yamepungua kwa kiasi kikubwa jambo ambalo limeleta matokeo chanya kutokana na nguvu kubwa na mikakati madhubuti iliyowekwa kwenye maeneo yaliyohifadhiwa na ushirikishwaji wadau katika masuala ya uhifadhi.

Hayo ni kwa mujibu wa Kaimu Mkurugenzi Msaidizi Sehemu ya Makosa ya Mazingira na Maliasili Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, Salimu Msemo alipozungumza na Waandishi wa Habari kutoka Chama cha Waandishi wa Habari za Mazingira Tanzania (JET) wanaotekeleza mradi wa USAID Tuhifadhi Maliasili  unaofadhiliwa na Shirika la USAID waliotembelea Ofisi ya Taifa ya Mashtaka mjini Dodoma hivi karibuni.

Msemo, alisema kuwa mkakati uliopo sasa ni kuendelea kuboresha namna za kupambana na ujangili kwasababu majangili nao wana mbinu mpya na mipango kwahiyo wao kama taasisi na wadau wengine wanajipanga kuona namna yakupambana nao.

“Sisi kama taasisi na wadau wetu wengine wa uhifadhi tunajipanga kuona namna ya kupambana na  majangili, teknolojia imekuwa kubwa kupata ushahidi ya utendekaji wa makosa haya, kuna namna nyingi sana teknolojia na mambo mengine inatumika kabla ya kufika kwenye kuua wanyama wetu,” alisema

Msemo aliongeza kuwa taasisi imeendelea kujiimarisha katika jitihada za utatuzi wa changamoto za ujangili na hatua zilizochukuliwa ili kudhibiti hali hiyo ni pamoja na Sheria na Adhabu: Muundo wa sheria umebadilishwa ili kuwa na adhabu kali kwa wale wanaovunja sheria za uhujumu uchumi na makosa ya wanyamapori. Mwaka 2016 sheria ya makosa ya uhujumu uchumi na makosa yakupanga, ilibadilishwa kwenye eneo la adhabu. Adhabu ya kifungo ni kati ya miaka 20 hadi 30, jambo ambalo linatisha wahalifu.

Ushirikiano wa Taasisi: Ofisi ya Taifa ya Mashtaka inafanya kazi kwa pamoja na vyombo vya sheria, polisi, na taasisi nyingine kama Shirika la la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) na Mamlaka ya Wanyamapori Tanzania (TAWA), ili kufikia mafanikio katika vita dhidi ya ujangili. Ofisi pia imekuwa ikitoa miongozo mingi inayowasaidia kupata ushahidi kutoka nje ya nchi.

Mafanikio ya Kiuchunguzi: Juhudi za uchunguzi na ukamataji wa wahalifu wa ujangili zimefanikiwa kwa kiasi kikubwa, na watu wengi wanaohusika na mitandao ya ujangili wapo gerezani.

Hii ni pamoja na kukamatwa kwa viongozi wa ngazi mbalimbali katika biashara hii. Lakini pia kufanikiwa kuwatia hatiani watu kwenye ile mitandao maana yake inapunguza nguvu ya mitandao na wakati mwingine kuna mitandao ambayo imekufa kabisa.

Suala hilo limepelekea nchi kuwa na taswira nzuri na wenzetu wanakuja kujifunza, hivi karibuni tumekuwa na wageni kutoka Msumbiji wamekuja kujifunza namna Tanzania inavyofanikiwa kwenye kupambana na makosa haya ya ujangili. Wengi wanakuja lakini na sisi pia tumekuwa tukijifunza kutoka kwao.

Mkakati Mpya: Kuna mpango wa kukabiliana na migongano kati ya wanyama na binadamu, ambapo hali ya wanyama inazidi kuimarika. Mikakati inaonekana kulenga kuboresha namna ya kupambana na changamoto hizi, ikiwa ni pamoja na teknolojia za kisasa kwa ajili ya uthibitishaji wa vitendo vya uhalifu.

 

Biashara ya Ujangili: Kulingana na ripoti zilizopo, nchi ya China ndio inaongoza katika biashara hii, huku meno ya tembo yakikamatwa mara nyingi.

Hii inaonyesha kuwa uhalifu huu unafanya kazi kwa mitandao ya kimataifa. Mchakato mzito wa kupambana na ujangili umeanza kuzaa matunda. Kwa kuimarika kwa sheria na adhabu kali, uhalifu wa ujangili umepungua tofauti na ilivyokuwa mwaka 2012 mpaka 2014, na hivyo kunatoa nafasi kwa wanyamapori kuongezeka.

Kwa upande mwingine, Msemo alisema kuwa hivi karibuni, kumekuwepo na ongezeko la wingi wa nyamapori katika maeneo mengi nchini Tanzania, ambayo yanaweza kuashiria mabadiliko katika matumizi ya rasilimali za wanyama.

“Kwa kawaida, wanyama kama swala, nyumbu na wengineo wanatumika kama chakula katika jamii, lakini hali hii inahitaji kuangaliwa kwa makini kwani inaweza kubeba changamoto na fursa mpya. Kwa kushirikiana na wadau, tunanaweza kuhakikisha kuwa rasilimali hizo zinatunzwa kwa faida ya kizazi cha sasa na kijacho,” alisema Msemo

Kwa ujumla, ujangili umepungua kwa juhudi za uhifadhi wa mazingira na maliasili. Ni muhimu kuendelea na mikakati hii ili kuhakikisha wanyama na mazingira vinapatikana na kuishi kwa usalama. 


 


 

Post a Comment

0 Comments