Ticker

7/recent/ticker-posts

MRADI WA KISIKI HAI NI MKOMBOZI WA MAZINGIRA

 

Wakina mama wakiweka alama kwenye maotea waliyochagua kwa kufunga kitambaa chenye rangi 

NA SIDI MGUMIA, DODOMA

Utunzaji wa mazingira ni juhudi za kulinda na kuhifadhi mazingira ili kuhakikisha kunakuwepo na uendelevu wa rasilimali asili na ustawi wa viumbe vyote.

Hii inahusisha shughuli na mikakati mbalimbali iyolenga kupunguza athari mbaya za shughuli za kibinadamu kwenye mazingira na kukuza matumizi endelevu ya rasilimali.

Moja ya vipengele muhimu vya utunzaji wa mazingira ni
hatua za kulinda, kudhibiti na kurejesha mifumo ya asili na iliyorekebishwa ambayo inashughulikia changamoto za jamii kwa ufanisi na wakati huo huo kunufaisha jamii.

Kwakulitambua hilo, Shirika lisilo la Kiserikali ya LEAD Foundation linalojihusisha na kukuza uongozi bora, utunzaji wa mazingira na maendeleo ya jamii, limejikita katika kurudisha mamilioni ya miti mkoani Dodoma kwa njia ya asili ya Kisiki Hai.

Akielezea njia hiyo kwa kina alipokuwa akizungumza na Waandishi wa Habari kutoka Chama cha Waandishi wa Habari za Mazingira Tanzania (JET) wanaotekeleza mradi wa USAID Tuhifadhi Maliasili  unaofadhiliwa na Shirika la USAID waliotembelea Ofisi za Shirika hilo mjini Dodoma hivi karibuni, Meneja Kumbukumbu na Mratibu wa mafunzo, Hagali Mbulla, alisema  Kisiki Hai ni njia ya kilimo msitu inayotumika ili kuotesha tena miti na kusaidia mimea mipya inayokua kwa asili kukua.

Meneja Kumbukumbu na Mratibu wa Mafunzo, Hagali Mbulla

Mbulla amesema, Kisiki Hai inajumuisha mchakato wa kuchagua, kupogolea na kulinda visiki vya
miti iliyokatwa. Kwa utunzaji sahihi, visiki hivi hupata nafasi ya kukua.

“Kwa kutumia njia ya Kisiki Hai na kuanzisha tena njia ya uvunaji wa maji ya mvua, tunakusudia kurejesha udongo, kulifanya eneo kuwa la kijani tena na kuboresha uzalishaji wa ardhi katika mkoa wa Dodoma, katikati mwa Tanzania,” alisema Mbulla

 Aliongeza kuwa njia ya Kisiki Hai imekuwa mkombozi wa mazingira hasa katika maeneo kame kwasababu kuu nne ambazo ni gharama nafuu, endelevu, rahisi kwa mtu yoyote kuifanya pia ina matokeo ya muda mfupi.

Mbulla amesisitiza kuwa wao wanajikita sana katika utunzaji wa mazingira kwa kutumia njia za asili kwa ajili ya kustawisha uoto wa asili, na hii ni baada ya tafiti zilizofanywa kuonyesha kuwa ndio njia sahihi ya kukuza miti katika maeneo yenye ukame.

Hali ilivyokuwa kabla na hali ilivyo sasa

“Tulianza kwa kutoa elimu mwaka 2017 na utekelezaji ulianza mwaka 2018 kwa Wilaya ya Kongwa na baadae wilaya ya Mpwapwa na baada ya matokeo mazuri ndipo tulipoanza kwenda na maeneo mengine,” aliongeza

“Hii miti tunayoitunza kwa njia ya asili tuna uhakika wa kuihudumia na baadae kuwa miti mikubwa kwasababu mpaka mwezi Juni mwaka huu 2024 tayari kuna miti milioni 22 imekua.

“Na katika kila kijiji tunachokwenda tunawafundisha wanakijiji wasiopungua wanne kulingana na ukubwa wa kijiji na lengo ni mkulima mmoja asimamie kaya 150, kwahiyo unakuta katika kila kijiji sasa tuna wakulima wanne ambao wamepewa mafunzo yakutosha halafu na wao wanakwenda kuwafundisha wenzao,” alisemaa Mbulla.

Alifafanua kuwa kwa wakulima waliopata mafunzo, hawatakuwa na kazi ya kuwafundisha wenzao tu bali kila mkulima anakabidhiwa kaya 150 za kuzisimamia, kila mwezi anakuwa anaripoti jinsi kazi inavyokwenda na kuorodhesha idadi ya miti waliyootesha kutoka kwa kila mkulima.

Waandishi wa Habari kutoka JET wakisikiliza maelezo kutoka kwa Meneja Hagali Mbulla

“Kiuhalisia hali imebadilika kwasababu hata ukiangalia historia kidogo ya Dodoma miaka ya zamani kabla ya 2000 ilikuwa ikifika Oktoba ama Novemba kulikuwa na kimbunga kikali kilichopewa jina la Kimbunga cha Kongwa kwasababu kilikuwa kinatoka maeneo ya Kongwa ambako hakuna miti mpaka kinafika mjini, lakini sasa hivi wenyeji wa Dodoma wanashangaa hawakioni kile kimbunga na hii ni kwasababu tayari miti imeshaongezeka huko, imekuwa ya kutosha kwahiyo upepo unazuiliwa na kuzuia hicho kimbuga,” alisema Mbulla   

Akiongelea kuhusu suala la ushiriki wa wanawake katika kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi kupitia mradi wa Kisiki Hai, ameeleza kuwa wanashiriki kikamilifu katika mradi huo na kwamba Shirika lao pia linazingatia zaidi suala la jinsia kwahivyo hata wakulima wale wanaowafundisha kule vijijini ni lazima kuwa na idadi sawa yani kama wanachukuliwa wanaume wawili katika kijiji basi na wanawake lazima wawe wawili.

“Katika utekelezaji wa miradi yetu kila siku bado tunawahimiza wanawake pia wawepo, na wanawake hawa sasa wanakiri kuwa wamepunguziwa adha ya kwenda kutafuta kuni mbali na hii ni kwasababu sasa akienda shambani kwake tu anarudi na mzigo wa kuni na sio kwenda mbali,” alisema Mbula

Pamoja na njia hiyo ya asili, wanatumia pia njia ya kuchimba mitaro ambayo inaitwa makinga maji ili kuyakinga maji na kuyahifadhi shambani, wanaitumia katika maeneo ya ukame. Maji yanayohifadhiwa hutumika mara baada ya mvua kukatika ambapo hunywea taratibu chini ya ardhi na kuifanya ibaki na unyevu.

Kwa upande wake Angelina Tarimo ambaye ni Afisa Ufuatiliaji, Tathimini na Kujifunza Ukijanishaji Kidijitali alisema kuwa mafaniko ya mradi ya Kisiki Hai yanaonekana na kwamba kwa upande wa kijiji cha Eslalei Wilayani Monduli, kijani imerudi kwa majani ya asili,wanyama lakini pia kurudi kwa mimea ambayo walikuwa wameshaisahau katika hilo eneo.

Afisa Masoko na Mawasiliano, Godlove Kihupi akifafanua jambo 

“Kutokana na kuwepo kwa miti mingi sasa wanyama waliotoweka kutokana na ukame wameanza kurudi. Wanyama hao ni digidigi, simbilisi, sungura na vipepeo,” alisema Tarimo

Nae Afisa Masoko na Mawasiliano wa shirika hilo, Godlove Kihupi alilisisitiza kuwa katika miradi yao ya utunzaji wa mazingira wametumia pia njia ya kuchimba mashimo ya umbo la nusu mwezi kwa ajili ya kukinga maji, wamefanya kwenye maeneo yenye ukame kwa mfano Wilaya ya Monduli kwenye kijiji cha Eslalei lakini wamefanya pia Meserani.

“Tunatumia mbinu za asili ambazo ni rahisi kutumika na jamii ambayo tunafanya nayo kazi,  lakini pia kwa kusikia maelekezo tu mtu anaweza akatekeleza zoezi hilo katika eneo lake. Na kwasasa maeneo ambayo tumekuwa tukiyaangazia zaidi ni kwenye ukame ili kusaidia kutunza maotea ya miti yanapochipua kutokana na Kisiki Hai au mbegu za miti zilizodondoshwa ardhini na vinyesi vya wanyama au ndege,” alisema Kihupi

Akielezea mafanikio ya mradi huo, mkazi wa kijiji cha Pembamoto, Dickson Saluni alisema kuwa kijiji chao kimekuwa na jangwa kwa muda mrefu lakini mambo yamebadilika mara baada ya kuja kwa mradi kwani sasa wamepata nyasi, miti na sasa kijiji chao kinapendeza.

Kwa upande wake Mariam Mungane ambae ni mkazi wa kijiji cha Pembamoto alisema kwasasa wanapata kipato kwa kuuza nyasi zinazoota kwenye maeneo yao na imewapunguzia adha kwenda mbali kutafuta kwakua sasa wanazipata kwenye mashamba yao wenyewe. 



Post a Comment

0 Comments