Ticker

7/recent/ticker-posts

TAWA: UJANGILI WA TEMBO UMEDHIBITIWA NCHINI

 


Ofisa Wanyamapori wa Kitengo cha Upelelezi kutoka Mamlaka ya Wanyamapori Tanzania (TAWA), Tryphone Kanon akifafanua jambo wakati wa mafunzo 

NA SIDI MGUMIA, BAGAMOYO

Tanzania imeendelea kupata mafanikio makubwa katika kuimarisha shughuli za uhifadhi kwa kutokomeza ujangili wa tembo na biashara haramu ya nyara katika maeneo yaliyohifadhiwa.

Mamlaka ya Wanyamapori Tanzania (TAWA) imesema kuwa eneo la ulinzi na usimamizi wa rasilimali za wanyamapori limeendelea kupata matokeo chanya kutokana na nguvu kubwa na mikakati madhubuti iliyowekwa kwenye maeneo yaliyohifadhiwa na ushirikishwaji jamii katika masuala ya uhifadhi.

Hayo ni kwa mujibu wa Ofisa Wanyamapori wa Kitengo cha Upelelezi kutoka Mamlaka ya Wanyamapori Tanzania (TAWA), Tryphone Kanon alipokuwa akizungumza katika mafunzo maalumu kwa waandishi wa habari yaliyoandaliwa na Chama cha Waandishi wa Habari za Mazingira Tanzania (JET) kupitia mradi wa USAID Tuhifadhi Maliasili unaofadhiliwa na Shirika la USAID.

“Kupungua kwa ujangili nchini kumechangiwa kwa kiasi kikubwa na kuendelea kuimarishwa ulinzi na kushirikiana na wadau mbalimbali sambamba na wananchi wanaoishi katika maeneo ya hifadhi ili kuidhibiti vikundi vya uhalifu dhidi ya wanyamapori kama tembo, faru na wengineo waliopo katika hifadhi mbalimbali za Taifa,” alisema Kanon

Ofisa huyo alisisitiza kuwa hali sasa ni tofauti na kuwa ripoti ya TAWA ya hivi karibuni imeonesha kuwa mauaji ya tembo yamepungua kutoka matukio 18 mwaka 2016 hadi matukio matatu mwaka 2023.

 

 “Kiwango cha ujangili wa tembo kimeshuka katika hifadhi za Taifa ukilinganisha na hali ilivyokua miaka ya nyuma. Kwa sasa meno ya tembo yanayokamatwa mengi ni ya miaka ya nyuma, na mapya yamekuwa ni nadra kuonekana, jambo ambalo linaonyesha kwamba mapambano dhidi ya ujangili yanazaa matunda,” alisema Kanon

Aliongeza kuwa kupungua kwa mizoga ya tembo iliyouawa na majangili kwenye maeneo mengi ya hifadhi nchini ndio kumeifanya TAWA kuamini kuwa sasa hali ni shwari. Lakini hawajaishia hapo bali wameendelea kuimarisha ulinzi na kujitahidi kudhibiti mitandao ya kijamii ambayo inatumika kama njia ya mawasiliano ya uhalifu wa wanyamapori.

Matokeo ya jitihada hizo za opereheni za TAWA ni kufanikiwa kuendelea kukamata watu waliohifadhi meno ya tembo ambapo kwa mwaka 2023 walikamatwa watu 3,700.

Pamoja na hilo, Kanon alizungumzia mbinu mpya ya ujangili wa kutumia mapanga ambao umeshamiri hivi sasa kuliko matumizi ya risasi kama ilivyozoeleka huko nyuma, ambapo muwindaji haramu humkata panga mnyama miguuni ili kumfanya ashindwe kutembea ama kukimbia hivyo inakuwa rahisi kumuua.

Risasi hazitumiwi sana kwa sasa kwasababu ni ghrama lakini pia ni kuogopa milio yake ambayo inaweza kuwashtua askari wanyamapori kwa haraka pia kuwashtua wanyama wegine na kuwafanya wakimbie, kitu ambacho ni changamoto kubwa kwa wawindaji haramu,”.

“Tawa tumebaini mbinu hiyo, hivyo nasi tunaimarisha ulinzi kwenye hifadhi zetu kuhakikisha kwamba hakuna majangili wanaofanikiwa katika mbinu zao za kuua wanyama,” alisisitiza Kanon

Kwa upande wake Dkt. Elikana Kalumanga ambaye ni Meneja wa ushirikishwaji wa sekta binafsi, mradi wa USAID Tuhifadhi Maliasili alisema ili kuweza kukabiliana na ujangili wa wanyamapori ni vyema kuwepo ushirikishwaji wa jamii na wadau wengine wa mazingira ili kusaidia juhudi za uhifadhi wa shoroba na mazingira kwa ujumla.

Dkt. Elikana Kalumanga, Meneja Ushirikishwaji wa Sekta Binafsi wa Mradi wa Shirika la Marekani la Maendeleo ya Kimataifa (USAID) wa Tuhifadhi Maliasili akiwasilisha mada ya uhifadhi wa wanyamapori

“Ushirikishwaji huo unapaswa kuwagusa wadau wote wa mazingira ili kuleta maendeleo endelevu ya malaisili zilizopo,” alisema Dkt. Kalumanga

Dkt. Kalumanga amesisitiza kuwa ikiwa wadau hao muhimu wakishirikiana kwa pamoja katika michakato mbalimbali ya usimamizi wa mazingira itasaidia kulinda, kuhifadhi, kutunza na kusimamia mazingira kwa ajili ya kizazi cha sasa na cha baadaye.

 

Akizungumza katika katika mafunzo hayo, Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Shule Kuu ya Uandishi wa Habari na Mawasiliano (SJMC), Dkt.. Abdallah Katunzi alisema kuwa waandishi wa habari haswa wanawake wana nafaasi kubwa ya kuelimisha umma kwa weledi juu ya masuala ya uhifadhi kwani wao ndio huguswa moja kwa moja na changamoto za uhifadhi.

Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Shule Kuu ya Uandishi wa Habari na Mawasiliano (SJMC), Dkt. Abdallah Katunzi akifafanua jambo katika mafunzo hayo

“Wanawake ni nguzo kubwa katika tasnia ya habari na italeta jita sana wakisaida katika kuripoti mambo ya ujangili wa wanyamapori kwasababu yale madhara yatokanayo na ujangili kwa namna moja au nyingine yanawakuta wao kwasababu wanahusika na hivi vitu, unakuta ni madhara kwa watoto na hata athari za kiuchumi mara nyingi zinawaumiza wanawake kwanza,” alisisitiza Dkt.. Katunzi

Pia kwakua jukumu hilo ni la waandishi wa habari, Dkt.. Katunzi amesisitiza iongezwe kasi ya kutoa elimu kwa wananchi kuhusu masuala ya uhifadhi na umuhimu wake kwa maendeleo ya vizazi vijavyo na Taifa kwa ujumla.

Naye Mkurugenzi wa JET, John Chikomo alisema kupitia mafunzo hayo yaliyoratibiwa na JET chini ya ufadhili wa USAID, yanalenga kuwapa waandishi wa habari za mazingira uelewa zaidi  juu ya masula ya uhifadhi wa wanyamapori na mazingira kwa ujumla wake ili kuandika habari kwa kina na iwe rahisi kufikisha ujumbe kwa ufasaha kwa jamii.

John Chikomo, Mkurugenzi wa  Chama cha Waandishi wa Habari za Mazingira Tanzania(JET)

“Tunaendelea kutoa elimu kwa waandishi wa habari kwasababu wanapaswa kuwa mstari wa mbele kuibua na kuelimisha jamii juu ya umuhimu wa kuwalinda wanyamapori, kutunza mazingira na kuzijua aathari zitokanazo na shughuli za kibinadamu kama kilimo na nyinginezo ndani ya shoroba pamoja na faida za kiuchumi zinazopatikana,” alisema Chikomo

Washiriki wa mafunzo ya Uhifadhi wa wanyamapori wakifuatilia mjadala kwa makini 



Post a Comment

0 Comments