Ticker

7/recent/ticker-posts

MAFURU: USHIRIKISHWAJI WA WADAU NI MUHIMU KATIKA KUYALINDA MAZINGIRA

 

Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Matumizi ya Ardhi, Joseph Mafuru 

NA SIDI MGUMIA, DODOMA

Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Matumizi ya Ardhi, Joseph Mafuru amesema ushirikishwaji wa wadau ni muhimu katika kuyalinda mazingira na kutekeleza kwa urahisi mipango ya matumizi ya ardhi nchini.

Mafuru ameyasema hayo alipokuwa akiongea na waandishi kutoka Chama Cha Waandishi wa Habari za Mazingira Tanzania ( JET), wanaotekeleza mradi wa Tuhifadhi Maliasili chini ya ufadhili wa Shirika la Marekani la Maendeleo ya Kimataifa (USAID), waliotembelea Ofisi za Tume ya Matumizi ya Ardhi mjini Dododma hivi karibuni.

Ameeleza kuwa wadau hao ambao ni wa uhifadhi, wananchi, taasisi za wanyamapori na wengineo wanapaswa kushirikishwa katika kuandaa mipango ya matumizi ya ardhi na kisha kusimamia kwa pamoja ili kurahisha utekelezaji.

“Ili uweze kuwashirkisha wadau, inafaa kuanza kuandaa mipango ya ardhi kwa pamoja na kisha mkaisimamia kwa pamoja hivyo kuitekeleza inakuwa ni rahisi sana. Usipowashirikisha utekelezaji wake utakuwa mgumu sana, kwahivyo kuna haja ya wadau wote kushiriki kwa pamoja kuhakikisha zoezi hilo linafanyika vilivyo,” alisema Mafuru

Aidha, Mafuru alisema kuwa kama Tume wanapambana kupata wadau wakutosha ili kuhakikisha wanaongeza kasi yakuandaa mipango ya matumizi ya ardhi. Vijiji vilivyoandaliwa mipango kwa sasa ni vichache sana ambapo ni vijiji 3000 tu kati ya vijiji 13,000 na hii maana yake bado kuna kazi kubwa yakufanya.

“Tukiongozwa na Serikali ikifuatiwa na wadau wengine kwenye masuala ya uhifadhi mazingira na wanyamapori, tunapaswa tuhakikishe tunatengeneza mipango yakutosha. Kwani kadri tunavyozidi kuchelewa kutengeneza maana yake tunaendelea kutengeneza migogoro kati ya wanyamapori na binadamu, hivyo ni heri tukaifanya mapema hiyo mipango ili kuepusha hiyo migogoro,” alisema Mafuru.

Kama Tume wameweka kwenye bajeti ya mwaka huu wa fedha unaoendelea wa 2024-2025, wametenga bilioni tano na zaidi kwa ajili yakuhakikisha kwamba kazi hizo zinafanyika kwa ufasaha. 

Mkurugenzi wa Utafiti na Uzingatiaji wa Mipango ya Matumizi ya Ardhi, Joseph Paul

Akizungumzia mafanikio ya kuwepo kwa mipango ya matumizi ya ardhi, Mkurugenzi wa Utafiti na Uzingatiaji wa Mipango ya Matumizi ya Ardhi, Dkt. Joseph Paul amesema, mipango ya matumizi ya ardhi imesaidia wanakijiji kutokuingia maeneo ya hifadhi lakini pia imesaidia kuongoa mapito ya wanyama na kuwafanya wapite kama ambavyo wanapaswa kupita.

“Kimsingi tunafahamu wanyama kama tembo huwa hawasahau njia zao, kwa kupitia Serikali za vijiji lakini pia wazee ambao wana uzoefu na maeneo hayo wamesaidia kuainisha maeneo ambayo yana umuhimu wa uhifadhi kuyatenga kwa matumizi rafiki ambayo hayatazuia wanyama kupita lakini shughuli za kibinadamu kuendelea,” alisema Paul

Paul alisisitiza kuwa mfano wa hilo ni upande wa Kaskazini ambapo mpango wa matumizi ya ardhi umesaidia katika kupanga matumizi nyanda za malisho kwa jamii ya kule.

Amesema kimsingi Tume ya Taifa ya Mpango wa Matumizi ya Ardhi imeratibu na kusaidia uandaaji wa mpango wa matumizi ya ardhi katika ngazi ya kanda, mkoa, kwa mfano ukanda ambao ni muhimu kwa uhifadhi kama mkoa wa Mara, mpango umeendelea kuandaliwa ili kuhakikisha kunakuwa na matumizi sahihi ya ardhi.

“Lakini pia tumegundua kwenye tafiti zetu kwamba ili tusaidie kusiwe na muingiliano wa kimatumizi kuna umuhimu wakuboresha maisha ya wananchi wenye maeneo yao. Moja ya njia za kuboresha ni kuhakikisha kwamba wana uhakika wa umiliki wa ardhi, kwahivyo tume imewezesha uandaaji hati miliki za kimila zaidi ya 20,000 kwa maeneo yenye umuhimu wa uhifadhi. Wanakijiji wa maeneo hayo wamepewa hati miliki za kimila kwa kuzingatia vigezo mbalimbali pamoja na kuhakikisha kuwa jinsia katika umiliki inazingatiwa, kwenye familia tumehakikisha mume na mke wanamilikishwa yale maeneo yao pamoja na kutenga maeneo kwa ajili ya uwekezaji wa ndani na nje ili kusaidia wananchi kutumia maeneo yao vizuri kwa kilimo na ufugaji wenye tija,” alisema Paul

Pamoja na hilo, Paul alisema kuwa ukosefu wa elimu ya matumizi bora ya ardhi bado ni changamoto kwa wanajamii, hivyo bado wanaendelea kuelimisha jamii juu ya umuhimu wa utunzaji na umuhimu wa utekelezaji mpango wa matumizi ya ardhi.

Ofisa Mkuu wa Ardhi wa Tume ya Mipango ya Matumizi ya Ardhi, Nyirembe Munasa

Kwa upande wake Ofisa Mkuu wa Ardhi wa Tume ya Mipango ya Matumizi ya Ardhi, Nyirembe Munasa alisema ili kuwe na maendeleo endelevu wanapendekeza kuwe na mipango ya matumizi ya ardhi katika mikoa yote nchi nzima, na kanda zilizopo mfano ikolojia ya ziwa Victoria, Tanganyika, Serengeti na kwingineko, inahitajika kuhifadhi maeneo ya ikolojia kwa kuzingatia matumizi ya ardhi katika ngazi za mikoa.

“Kuna umuhimu mkubwa sana kulinda mifumo ya ikolojia, lakini nchi yetu ina mifumo mingi ya ikolojia ambayo hailindwi hasa hizi shoroba ambazo wanyama hutumia kutoka kwenye hifadhi moja kwenda nyingine. Kwa bahati mbaya sana unakuta miongoni mwa hizi shoroba nyingi sana zimezibwa kwa aidha shughuli za kilomo au makazi ya binadamu jambo linalosababisha migongano kati ya wanyama na binadamu. Hakukuwa na mikakati au mipango ambayo ilikuwa inaelekeza namna gani hayo maeneo yahifadhiwe. Lazima tufanye uongoaji wa hizi shoroba kwa kutumia mipango shirikishi ya matumizi ya ardhi, kuwe na maendeleo endelevu sababu yana umuhimu wake kuchumi, kijamii na pia katika mambo ya mazingira na kiikolojia,” alisema Munasa

Aliongeza, “Kuhusu shoroba ziko 66 lakini ni mbili tu ndizo zimefanyiwa kazi ikiwemo shoroba ya Ifakara. Changamoto kubwa iliyokwamisha zoezi hili ni fedha na hii ni kwasababu shoroba ziko nyingi na tunahitaji kuwa na mipango ya matumizi katika vijiji vyote vinavyopitiwa na shoroba,”.

Mkurugenzi Msaidizi Uzingatiaji wa Mipango ya Matumizi ya Ardhi, Rehema Kishoa

Nae Mkurugenzi Msaidizi Uzingatiaji wa Mipango ya Matumizi ya Ardhi, Rehema Kishoa ameongeza kuwa kama hakuna usimamizi mzuri hizo shoroba hazitakuwepo, mipango itapangwa lakini  hazitakuwepo, kwahiyo ni vyema kuangalia namna yakuwashirikisha wananchi wakati mipango inaandaliwa kwasababu wao ndio wahusika wakuu katika suala zima la kuwepo ama kutokuwepo kwa shoroba hizo.  

“Tume ina wajibu wakuhakikisha mipango ya matumizi ya ardhi inayoandaliwa kwa ngazi zote inasimamiwa kama ilivyopangwa. Muhimu kwa wanajamii, watalaamu na wadau wengineo kushirikiana juu ya masuala ya ardhi,” alisema Kishoa

Mkurugenzi wa Chama Cha Waandishi wa Habari za Mazingira Tanzania ( JET), John Chikomo (wa tatu kutoka kulia) akielezea jambo wakati wa majadiliano.

Hata hivyo, Mkurugenzi wa JET, John Chikomo ameongeza kuwa katika mapambano dhidi ya changamoto za mabadiliko ya tabia nchi elimu ya mazingira na haswa uhifadhi bado inahitaji ipelekwe kwenye jamii lakini pia kusisitiza uwepo wa ushirikishwaji wa sekta na wizara mbalimbali katika masuala ya mazingira.

Waandishi wa habari za mazingira kutoka vyombo mbalimbali nchini waliotembelea ofisi za Tume ya Matumizi ya Ardhi

“Ikiwa wadau muhimu kama vile Wizara ya Maliasili na Utalii, watunga sera, waandishi wa habari na wengineo watashirikiana kwa pamoja katika maandalizi ya sera, mipango na michakato ya usimamizi wa mazingira itasaidia kulinda, kuhifadhi, kutunza na kusimamia mazingira kwa ajili ya kizazi cha sasa na cha baadae,” alisema Chikomo

 


Post a Comment

0 Comments