Ticker

7/recent/ticker-posts

UHABA WA UTAFITI KIKWAZO SHUGHULI ZA UTALII

 



Afisa Uhifadhi kutoka Mamlaka ya Wanyamapori Tanzania (TAWA) ambaye pia ni Msimamizi wa Utalii Huduma za Biashara, Kanda ya Dar es Salaam, Weja Lugendo


Na Sidi Mgumia, Dar es Salaam

Uhaba wa utafiti wa soko unatajwa kuwa moja ya vikwazo vikubwa katika sekta ya utalii nchini haswa katika kukabiliana na ushindani kibiashara.

Hayo yameelezwa na Afisa Uhifadhi kutoka Mamlaka ya Wanyamapori Tanzania (TAWA) ambaye pia ni Msimamizi wa Utalii Huduma za Biashara, Kanda ya Dar es Salaam, Weja Lugendo, wakati wa kujadili masuala ya uhifadhi wa bioanuai.

Mjadala huo uliandaliwa na Chama cha Waandishi wa Habari za Mazingira Tanzania (JET) kwa kushirikiana na Shirika la Marekani la Maendeleo ya Kimataifa (USAID) kupitia mradi wake wa Tuhifadhi Maliasili.

Lugendo amesema kuwa kutokuwepo kwa utafiti wa kutosha ni moja ya changamoto kubwa kwani ni vigumu kufahamu soko la biashara ya utalii nje na ndani linataka nini lakini pia kunapelekea shughuli za utalii kushindwa kufanya vizuri katika ngazi tofauti.

“Kiukweli utafiti wa soko ni eneo lenye changamoto, ukiangalia Tanzania kwenye hizi taasisi zetu hatufanyi tafiti za kupata kujua masuala kama fursa za uwekezaji kwa maana ya wapi tukawekeze na mengineyo lakini pia kuzifahamu changamoto zilizopo ambazo zikibainika kwa wakati ni rahisi kuzifanyia kazi na kuepusha vikwazo katika sekta nzima ya utalii,” alisisitiza Lugendo

Pamoja na hilo, alisema pia kuna changamoto ya serikali kutokuwa na fedha za kutosha kwa ajili ya kuutangaza utalii, na wao kama sehemu ya serikali wanakwama katika utekelezaji kwakua fedha za serikali zinaeleweka kuwa sio nyingi.

“Kingine ni kwamba kuna vivutio vichache, hivyo kunahitajika kuwe na mwendelezo wa vivutio ili wageni wakija wasiishie kuona wanyama tu bali kuwe na mambo mengine kama vile ya utamaduni na mengineyo ambayo yatawafanya kuona vitu vipya kila mara wanaporudi kutembelea maeneo yetu.”

Afisa huyo aliongeza kuwa bado kuna changamoto katika miundombinu, ili kuwavutia wateja ni lazima uwe mbunifu kwenye biashara yako na kufanya uboreshaji wa miundombinu ya utalii kama vile hoteli, barabara, viwanja vya ndege na huduma pia za kitalii, uboreshaji ambao utaisaidia sekta ya utalii kutimiza lengo lake la kufikisha watalii milioni 5 na dola bilioni 6 ifikapo 2025.

Akizungumzia mapambano dhidi ya ujangili, Msafiri Kasara ambaye ni Mhifadhi Mwandamizi kutoka Mamlaka ya Wanyamapori Tanzania (TAWA) Kanda maalum ya Dar es Salaam, amesema bado wanaendelea kushinikiza matumizi ya sheria juu ya udhibiti wa usafirishaji wa nyara zinazongia na kutoka nchini lakini pia kushirikiana kwa karibu zaidi na serikali, baadhi ya taasisi zinazojihusisha na uhifadhi nchini pamoja na wananchi, yote haya ni hakikisha wanadumisha ushirikiano na kudhibiti ujangili.



Msafiri Kasara Mhifadhi Mwandamizi kutoka Mamlaka ya Wanyamapori Tanzania (TAWA) Kanda maalum ya Dar es Salaam akisisitiza jambo wakati wa majadiliano

 “TAWA tunazielimisha jamii zinazozunguka maeneo ya uhifadhi juu ya faida za uhifadhi wa wanyamapori na mazingira yake, tumefikia mpaka hatua ya kutoa gawio kwa vijiji ambavyo vipo katika maeneo ambayo watalii wanawinda, tunawapatia asilimia 25 ya pato linalopatikana katika pori husika kila mwaka. Lakini pia tunajenga shule, watoto wanasomeshwa katika yale maeneo, wanapelekwa kwenye vyuo vya uhifadhi na huduma nyingine nyingi,” alisema Kasara

Aliongeza kuwa, “Kufanya hivyo kunasaidia wananchi kuthamini uhifadhi wa wanyamapori na mazingira kwa ujumla lakini pia kutofanya ujangili, na mpaka sasa tayari shilingi bilioni 37 zimetumika kwa ajili ya malipo hayo,”

Akiwasilisha mada inayohusu changamoto ya viumbe vamizi katika uhifadhi na maendeleo ya jamii, Joseph Olila ambaye ni Meneja wa Kitengo cha Sera za Usimamizi wa Maliasili katika mradi wa USAID Tuhifadhi Maliasili,  amesema kuwepo kwa viumbe vamizi kwenye uhifadhi kumekuwa miongoni mwa sababu inayochagia kuathiri mazingira na kufifisha kasi ya ongezeko la vivutio vya utalii nchini.

Olila amesema viumbe vamizi vinahusisha aina ya mimea, wanyama au kiumbe chochote kile kinapoingia sehemu kwa  mara ya kwanza na kuleta uharibifu.

“Kimazingira kiumbe vamizi kina tabia ya kuondoa viumbe vya asili na chenyewe kutawala eneo husika jambo linalosababisha kuleta madhara ya uharibifu  wa uoto wa asili, hatua hii inaathiri viumbe vilivyopo.”


Washiriki wa mjadala juu ya masuala ya uhifadhi wa bioanuai

Aidha amezitaja changamoto nyingine kuwa ni pamoja na kupoteza tamaduni, ufugaji, magonjwa kwa binadamu, kupoteza mali kama mazao na mifugo, kwenye biashara lakini pia kwa serikali kutumia fedha nyingi kudhibiti, kusimamia, kupunguza uzalishaji jambo ambalo husababisha kupanda kwa bei za vyakula na nyingine nyingi.   

“Changamoto ni nyingi ikiwemo ya Utalii ambao unaathirika sana, hii ni kwasababu viumbe vamizi wanaposababisha uharibifu wa mazingira kwa kipindi kirefu, wanyama wanapungua jambo ambalo linapunguza watalii kwani mazingira asili yanakuwa yametoweka,” amesema Olila.



Adda Ngoya, Mkuu wa Kitengo cha mawasiliano-USAID

Olila aliongeza kuwa katika kukabiliana na changamoto hiyo jitihada nyingi zinafanyika lakini pia Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais, Mazingira iliandaa Mpango Mkakati wa Taifa wa kukabiliana na viumbe vamizi wa miaka 10 ambao umeanza mwaka 2019 hadi 2029.

Akiongelea juu ya uwepo wa sera na sheria za uhifadhi, John Noronha ambaye ni Meneja Ufuatiliaji kutoka Mradi wa USAID Tuhifadhi Maliasili alisema sheria zipo na zinasaidia lakini zina mapungufu jambo ambalo ni changamoto kwenye suala zima la uhifadhi wa wanyamapori na mazingira kwa ujumla.   

“Sheria zipo lakini bado kuna changamoto ya upungufu katika sheria hizo, hivyo basi ni vyema serikali izipitie na kuziongeza mfano: ni suala la mtu aliyelima kwenye kingo ya hifadhi, hafidiwi, vitu kama hivi na vingine vinapaswa kuangaliwa kwa umakini,” amesema.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa JET, Dkt. Ellen Otaru amesema kuwakutanisha pamoja waandishi wa habari na wataalamu wa mazingira ni suala muhimu kwasababu ni njia sahihi yakufanya majadiliano ya kina juu ya masuala ya bioanuai na uhifadhi kwa ujumla lakini pia kujifunza ili kwa pamoja kuweza kupata kilichokusudiwa ikiwa ni mwendelezo wa sehemu ya utekelezaji wa mradi wa USAID Tuhifadhi Malisasili.

           Mwenyekiti wa JET, Dkt. Ellen Otaru akifafanunua jambo wakati wa mjadala 

“Mafunzo ya bioanuai ni muhimu sana katika masuala yote ya uhifadhi wa mazingira, na kama waandishi kazi yetu kubwa ni kuzishirikisha, kuzifundisha jamii juu ya umuhimu wake lakini pia taarifa zetu tunazoziandaa zinachangia kuhakikisha kwamba sera, miongozo, mikakati iliyopo ndani na nje ya nchi zinatekelezwa, wananchi wanazielewa na wanazitekeleza lengo likiwa ni kuleta mabadiliko chanya kwa wananchi katika masuala yote ya uhifadhi wa bioanuai,” alisema Dkt. Otaru      

  


Post a Comment

0 Comments