Ticker

7/recent/ticker-posts

UANDISHI WA USHAHIDI NA KIJINSIA: SILAHA DHIDI YA ATHARI ZA TABIANCHI

 

Teresa Anderson, Kiongozi wa Kimataifa wa Haki ya Tabianchi kutoka ActionAid International
NA. SIDI MGUMIA, DAR ES SALAAM
“Wanahabari wanapaswa kuandika habari zenye kuleta mabadiliko kwa jamii, ziwe na ushawishi wa kisera badala ya kuwa taarifa za kawaida,” anasema Teresa Anderson, Kiongozi wa Kimataifa wa Haki ya Tabianchi kutoka ActionAid International.

Akiwasilisha mada kuhusu matokeo ya COP30 na dhana ya mpito wa haki katika mabadiliko ya tabianchi, Anderson amesisitiza kuwa vyombo vya habari vina nafasi ya kipekee kusukuma ajenda ya haki ya tabianchi kwa kutumia ushahidi, takwimu na uchambuzi wa kina. 

Anasema mataifa yanayoathirika zaidi na mabadiliko ya tabianchi yana mchango mdogo katika uchafuzi wa mazingira, hivyo nchi tajiri zinapaswa kupunguza uzalishaji wa gesi joto na kuongeza ufadhili wa kukabiliana na athari hizo.

Kauli hiyo imetolewa katika mafunzo ya uandishi wa habari za tabianchi yaliyoandaliwa na Media for Environment, Science, Health and Agriculture (MESHA) kwa kushirikiana na International Development Research Centre (IDRC), yakihusisha wanahabari kutoka Tanzania, Kenya, Uganda, Zimbabwe, Zambia na Malawi kupitia programu ya Cross Border Science Café.

AFRIKA NA MZIGO WA ATHARI ZA TABIANCHI

Wakati Afrika ikiendelea kuwa miongoni mwa maeneo yanayoathirika zaidi kwa mafuriko, ukame na mabadiliko yasiyotabirika ya mvua, wadau wa mazingira wameona umuhimu wa kuwawezesha wanahabari kuripoti kwa kina masuala hayo. Lengo ni kuhakikisha jamii zinaelewa chanzo cha changamoto na kushiriki kikamilifu katika suluhisho.

Kwa mujibu wa Anderson, uandishi wa tabianchi lazima uweke mbele haki za jamii zilizo hatarini zaidi, na ufuatilie kwa karibu ahadi na sera zinazotolewa katika mikutano ya kimataifa ya tabianchi kama COP. Amesema pia kuwa kiwango cha fedha kinachotolewa kupitia Mfuko wa Hasara na Uharibifu (FRLD) hakilingani na mahitaji halisi, akieleza kuwa dola milioni 250 zilizotengwa ni ndogo ukilinganisha na hitaji la takribani dola bilioni 395 kwa mwaka.

TABIANCHI,JINSIA NA AFYA NI MZIGO KWA WANAWAKE

Mabadiliko ya tabianchi si suala la mazingira pekee, bali pia ni la kijinsia na kiafya. Wataalamu wanasema wanawake na wasichana huathirika zaidi kutokana na mifumo ya kijamii inayowaweka katika hatari kubwa wakati wa majanga ya kimazingira.

Uhaba wa maji bado ni changamoto kwa wanawake wengi Afrika 

Meneja wa Mawasiliano wa Mission Inclusion, Audrey Masitsa, anaeleza kuwa ukame na upungufu wa mvua husababisha wanawake kutembea umbali mrefu kutafuta maji na kuni, hali inayowaweka katika hatari ya ukatili wa kijinsia na changamoto za kiafya. Anasisitiza kuwa mawasiliano yenye ushahidi yanaweza kuhamasisha hatua za haki na kubadili simulizi potofu zinazowaonyesha wanawake kama wahanga pekee.

Badala yake, wanawake pia wanaongoza suluhisho. Katika baadhi ya maeneo, wamekuwa mstari wa mbele kusimamia mikoko na miradi ya uhifadhi wa mazingira, hatua inayochangia kulinda fukwe, kuimarisha kipato na kukuza uongozi wao katika jamii.

Wanawake wakishiriki katika shughuli za uhifadhi wa mazingira kwa kupanda mikoko wilayani Pangani, mkoani Tanga

Kwa upande wake, Kiongozi wa Mkakati na Masuala ya Kiufundi kutoka African Centre for Health, Climate and Gender Justice Alliance (ACHCGA), Imali Ngusale, anasema ushirikiano kati ya wataalamu na vyombo vya habari ni muhimu katika kuhakikisha taarifa sahihi za kisayansi zinafika kwa umma na kwamba ahadi za serikali zinatekelezwa.

WAJIBU WA VYOMBO VYA HABARI

Washiriki wa mafunzo hayo wamekubaliana kuwa uandishi unaozingatia jinsia si utetezi bali ni wajibu wa kitaaluma unaolenga kutoa taarifa kamili na zenye muktadha. Wanahabari wametakiwa kuongeza uchunguzi kuhusu matumizi ya fedha za tabianchi, kufuatilia utekelezaji wa sera, na kuandika simulizi zinazoonesha suluhisho pamoja na changamoto.

Katika kipindi ambacho mabadiliko ya tabianchi yanaongeza ukosefu wa usawa, hasa kwa wanawake, vyombo vya habari vina jukumu la kubadili mwelekeo wa simulizi kutoka kwa taarifa za kawaida hadi habari za ushahidi, uwajibikaji na ushawishi wa kisera.

Kwa kufanya hivyo, uandishi wa habari unaweza kuwa kichocheo cha haki ya tabianchi, usawa wa kijinsia na maendeleo endelevu barani Afrika.

 


Post a Comment

0 Comments