Ticker

7/recent/ticker-posts

KAMA JAKAYA NA UHURU, KAMA RIDHIWANI NA JOMO

KAMA JAKAYA NA UHURU, KAMA RIDHIWANI NA JOMO 

 JAKAYA Kikwete, Rais wa Nne Tanzania. Uhuru Kenyatta; Rais wa Nne Kenya. 

 Ridhiwani ni mtoto wa kwanza wa Jakaya. Jomo ni mwana wa kwanza wa Uhuru. 

 Jana, Julai 21, 2023, ikiwa ni chini ya mwaka mmoja tangu Uhuru akabidhi hatamu ya nchi kwa William Ruto, Jomo, alivamiwa na maofisa usalama. 

 Mwaka 2017, ikikaribia miaka miwili tangu Jakaya alipokabidhi urais kwa John Magufuli, Ridhiwani, alipokea wito wa maofisa usalama. 

 Tuhuma za Jomo; kumiliki silaha bila kibali. Tuhuma za Ridhiwani; dawa za kulevya. Ridhiwani, baada ya kupokea wito, alimjulisha Jakaya ambaye alikuwa nje ya nchi. 

 Jomo, baada ya kuvamiwa na maofisa usalama, alimpigia simu Uhuru. Jakaya, baada ya taarifa alishituka, akauliza: “Tumefika huku kweli?”

 Baada ya mshituko, Jakaya alimwambia Ridhiwani: “Nenda, you'll keep me posted.” 


Uhuru alimuuliza Jomo, maofisa hao walikuwa na utambulisho gani? Jomo alijibu, wamesema wanatoka ofisi ya Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI) na magari wanayotumia yana namba za usajili wa Sudan.

 Uhuru alimwambia Jomo: “Usifungue geti, nakuja.” Maofisa wale waliondoka kabla Uhuru hajafika.

 Niliwahi kumuuliza Ridhiwani, alipoitikia wito huo aliambiwa nini? Alisema, alipofika alipewa kahawa anywe. 

Mkuu wa wale maofisa akamduwaza, alipomwambia: “Baba yako kabla hajatoka madarakani, alituagiza tukuchunguze kama unahusika kweli na dawa za kulevya. Alitwambia, kama ni kweli, bora akufunge mwenyewe au akusamehe yeye mwenyewe. 

 “Baba yako alitwambia, ingemuuma sana angetoka madarakani, uje ukamatwe na ufungwe. Tulikuchunguza. 


 “Bahati yako hatukubaini chochote, vinginevyo ungepambana na baba yako. Huu wito wa sasa ni siasa zenu. Sisi hazituhusu, maliza kahawa nenda zako.” 

Uhuru, yeye alitinga mzimamzima nyumbani kwa Jomo, Karen, Nairobi. Akasema mbele ya wanahabari: “Kukaa kwangu kimya wanadhani naogopa. Achaneni na familia yangu, nifuateni mimi. Nipo!” 

 Ni visa na mikasa inayofanana ya marais na warithi wao. Visasi vina nguvu kuliko kuhudumia wananchi. Angola, familia ya Eduardo Santos, ilihama nchi baada ya kutoka madarakani. Nchi yao, wanaogopa kurudi. 

 Ndimi Luqman MALOTO

Post a Comment

0 Comments