Ticker

7/recent/ticker-posts

BRELA YAOMBWA KUSAIDIA VIJANA WA TEMEKE KURASIMISHA BIASHARA ZAO

Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), imesisitizwa kusaidia vijana wa Wilaya ya Temeke ili waweze kurasimisha biashara zao. 

Kauli hiyo imetolewa na Mhe. Abdallah  Mtinika, Mstahiki Meya wa Halmashauri ya  Wilaya ya Temeke alipotembelea banda la BRELA kwenye Maonesho ya Kijana Janjaruka Festival Temeke ya Fursa leo tarehe 21 Mei, 2023 katika uwanja wa Zakhiem Mbagala. 

Mhe. Mtinika ameiomba BRELA isaidie vijana katika kutoa mafunzo mbalimbali ili waweze kutumia fursa zilizopo wilaya ya Temeke 

"BRELA muandae programu mbalimbali za kuwashirikisha vijana wa Temeke ili waweze kutoka kwenye utegemezi na kufikia hatua ya kujisimamia kwa kuwa    fursa zipo nyingi" amesisitiza Mhe. Mtinika.


Naye Nassoro Mtavu, Msaidizi wa Usajili Mwandamizi kutoka BRELA, ameeleza kuwa BRELA inatoa mafunzo kuanzia ngazi za vyuoni na pia wale walio nje ya mfumo wa elimu,  huwafikia kwa kushiriki kwenye matukio mbalimbali yanayoratibiwa kuanzia ngazi za wilaya. 

"Kwa upande wa vyuoni vijana wamekuwa na bunifu zao bila ya kujua namna ambavyo wanaweza kuzilinda bunifu hizo na kuzitumia kibiashara" amesema Mtavu 

Mtavu amesisitiza kuwa BRELA imeweza kutambua mchango wa vijana hao hasa kupitia maadhimisho ya siku ya Miliki Ubunifu Duniani ambapo Tanzania iliadhimisha Aprili 28,2023 kupitia alama zao  walizosajili, BRELA ilitambua ubunifu wao na kuwatunukia tuzo ikiwa ni sehemu ya kuthamini mchango wao katika ukuaji wa sekta ya biashara nchini, kutoa ajira na kuwepo kwa alama ya biashara ambayo bidhaa yake imedumu kwenye soko la biashara kwa muda mrefu

BRELA inashiriki kwenye maonesho ya Kijana Janjaruka Festival Temeke ya Fursa kwa kutoa huduma mbalimbali za Sajili, utoaji wa Leseni na huduma baada ya Sajili. Maonesho haya yanatarajiwa kufungwa Mei 24, 2023.

Post a Comment

0 Comments